Rwanda Wampongeza Rais Magufuli Kwa Kutumbua MAJIPU Bandarini.
WAFANYABIASHARA
wa Rwanda wamepongeza hatua zinazochukuliwa na Rais John Magufuli
katika Bandari ya Dar es Salaam, kwa kuimarisha ufanisi wa bandari,
kukuza biashara baina ya Tanzania na nchi jirani.
Aidha
wamesema tangu Rais Magufuli aanze kuchukua hatua hizo, mizigo yao
imekuwa salama zaidi na wamefanikiwa kuipata kwa urahisi tofauti na
zamani ambapo mingi ilikuwa ikipotea.
Hayo
yalielezwa jana na Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika
Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi Augustine Mahiga wakati
akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA).
Akizungumza
baada ya kutua nchini akitokea Kigali, Rwanda, Balozi Mahiga alisema
pia Rais wa nchi hiyo, Paul Kagame amemhakikishia kuwa ataendelea
kushawishi wafanyabiashara wake kutumia Bandari ya Dar es Salaam, ili
kukuza uhusiano wa kibiashara uliopo.
“Nilipata
bahati ya kuzungumza na wafanyabiashara wa kule... wamepongeza sana
hatua zinazochukuliwa na Rais Magufuli pale bandarini kwa sababu
wanasema sasa hivi itawasaidia sana kuhakikisha usalama wa mizigo yao,” alisema Blozi Mahiga.
Alisema
wafanyabiashara hao pia wameomba mkutano wa pamoja na wenzao wa
Tanzania, ili kujadili masuala mbalimbali, ikiwemo fursa za uwekezaji
ndani ya Rwanda na Tanzania.
Alisema
Rais Kagame anaunga mkono ujenzi wa reli itakayotumika kusafarisha
mizigo kwa kuwa ni njia mojawapo ya kukuza uchumi wa nchi hizo mbili
rafiki.
Akizungumzia
safari yake hiyo, Balozi Mahiga alisema, alienda nchini humo
kujadiliana masuala mbalimbali aliyoagizwa na Rais Magufuli kwa Rais wa
nchi hiyo, ambapo walijadili masuala matatu, ikiwemo machafuko
yanayoendelea Burundi.
Alisema
kuhusu machafuko ya Burundi, Rais Kagame alikanusha tuhuma zinazotolewa
na nchi hiyo pamoja na jumuiya za kimataifa kuwa anahusika katika
kuchochea machafuko hayo.
Kwa
mujibu wa Balozi Mahiga, maandamano ya nchi nzima yaliyofanyika wiki
iliyopita nchini Burundi ya kuishutumu Rwanda kuhusika na machafuko
nchini mwao, yalishitua nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC),
kutokana na baadhi ya maneno ya chuki yaliyokuwa yakitolewa na wananchi
hao dhidi ya nchi hiyo.
Alisema hali hiyo, ilihofiwa kwamba ingeweza kuvunja mazungumzo ya kutafuta suluhu yanayoendelea. “Nilimuuliza
Rais Kagame kuhusu hili suala, akasema hatachukua hatua yoyote licha ya
kwamba wananchi wake wamemlazimisha kufanya kitu."
Lakini alisema atashiriki katika majadiliano ya kutafuta suluhu ya Burundi.
“Sisi tulikuwa tunahofia kuwa huenda akachukua hatua ambazo zingeweza
kuleta matatizo na hata mazungumzo yanayoendelea kuvunjika, lakini
ameniambia hatachukua hatua yoyote inayoweza kusababisha kuvunjika kwa
uhusiano,” alisema Balozi Mahiga.
Hata
hivyo, alisema Rais Kagame alilalamikia nchi yake kushutumiwa kwa kutoa
mafunzo ya kijeshi kwa wakimbizi wa Burundi, ili kuipindua Serikali ya
nchi hiyo na kutaka Jumuiya za Kimataifa, kuwaondoa wakimbizi zaidi ya
70,000 na kuwahamishia nchi nyingine za jirani.
“Aliniambia
kuwa kuendelea kuwa na hawa wakimbizi katika nchi yake, kunaweza
kumletea matatizo makubwa, kwa sababu amekuwa akilaumiwa sana. Hivyo
kuliko lawama, ni bora hizi Jumuiya za Kimataifa zikawaondoa wakimbizi,” alisema.
Alisema
kwa mujibu wa Rais Kagame, Rwanda itaendelea kushiriki katika mijadala
mbalimbali ya kutafuta suluhu ya Burundi na itahakikisha Burundi inakuwa
salama.
Jambo
lingine walilozungumza na Rais Kagame ni mkutano wa marais wa Nchi za
Jumuiya ya Afrika Mashariki, unaotarajiwa kufanyika mwisho wa mwezi
nchini Tanzania, ambapo pia alikuwa katika hatua ya mwisho katika
kukamilisha ajenda na watakaoshiriki mkutano huo.
Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Ernest Mangu Atangaza Oparesheni Kamata Bodaboda Nchi Nzima
MKUU
wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Ernest Mangu amewaagiza makamanda wa
Polisi kote nchini, kuendesha oparesheni kali ya kuwachukulia hatua za
kisheria, waendesha bodaboda wasiotii sheria za usalama barabarani.
Ametaja
makosa yatakayosababisha waendesha bodaboda hao kukamatwa kuwa ni
pamoja na kubeba abiria zaidi ya mmoja, kupita katika taa nyekundu na
kutovaa kofia ngumu.
IGP
Mangu alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na maofisa wakuu wa Polisi,
wakiwemo makamanda wa Polisi wa mikoa, vikosi na makao makuu katika
kikao kazi kilichofanyika Dar es Salaam hivi karibuni ambacho
kilifunguliwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga.
Alisema
waendesha bodaboda wamekuwa wakikaidi kufuata sheria za usalama
barabarani, lakini sasa mwisho wao umefika na kuwataka makamanda wa
Polisi wa mikoa kote nchini, kutekeleza maelekezo hayo, ili kuleta
nidhamu kwa bodaboda katika kufuata sheria za usalama barabarani.
IGP
Mangu alisema suala la kufuata sheria za usalama barabarani kwa
bodaboda halina mjadala na kila Kamanda ahakikishe kuwa wote wasiofuata
sheria na kukaidi, wanakamatwa bila kuoneana muhali kwa kuwa wamekuwa
wakisababisha ajali zinazoweza kuzuilika.
“Pamoja
na kuendelea kudhibiti uhalifu wa aina zote, natoa maelekezo kwa kila
mkoa kuhakikisha unaendesha oparesheni kali dhidi ya bodaboda, ili
kupunguza ajali zinazosababishwa na bodaboda.
“Wengi
wao hawataki kufuata sheria na kanuni za usalama barabarani, tusiwaonee
muhali maana maisha ya watu ni muhimu sana na jambo la msingi ni
kusimamia sheria tu,” alisema IGP Mangu.
Awali
akifungua kikaokazi hicho Waziri Kitwanga alilitaka Jeshi la Polisi
kuendelea na mapambano yake dhidi ya uhalifu na wahalifu, ili usalama wa
raia na mali zao uendelee kuimarika na Watanzania waendelee na shughuli
zao za kujiletea maendeleo bila hofu ya kutendewa uhalifu.
Waziri Mkuu Atinga Bandari Ya Tanga....Akutana Na MADUDU Kibao
WAZIRI
MKUU Kassim Majaliwa jana jioni (Ijumaa, Februari 19, 2016) alikagua
bandari ya Tanga na kumtaka Mkuu wa Bandari ya Tanga (Port Master), Bw.
Henry Arika amletee maelezo juu ya ukiukwaji wa manunuzi ya tishari
ifikapo leo (Jumamosi) saa 6 mchana.
Waziri
Mkuu ambaye aliwasili Tanga jana mchana ili kushiriki mazishi ya baba
mzazi wa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto,
Bi. Ummy Mwalimu yaliyofanyika kwenye makaburi ya Mchukuuni, Tanga,
aliamua kuzuru bandari hiyo kabla ya kuelekea uwanja wa ndege akiwa njia
njiani kurejea Dar es Salaam.
Katika
ziara hiyo fupi, Waziri Mkuu alikataa kuingia ofisini (bandarini) na
akataka apelekwe mahali tishari tatu za bandari hiyo zilipo.
Katika
maswali aliyoulizwa na Waziri Mkuu, Bw. Arika alikiri kuwa matishari
hayo hayafanyi kazi kama inavyotakiwa kwa sababu yanasubiri kusukumwa na
tugboat (meli ndogo).
"Nataka
kesho saa 6 mchana uniletee barua yenye maelezo ni kwa nini mlinunua
tishari tatu ndogo badala ya mbiili kubwa wakati mnajua Serikali
ilitenga Dola za Marekani milioni 10.113 kwa ajili ya kununua tishari
mbili zenye uwezo wa kujiendesha zenyewe (self propelled) "
“Nataka
maelezo ni kwa nini mlizinunua tangu mwaka 2011 lakini zimekaa bila
kufanya kazi hadi Novemba mwaka jana? Na kwa nini mnaendelea kutumia
hela ya Serikali kwa kukodisha tishari kutoka Mombasa badala ya
kutengeneza za kwenu au kufundisha vijana wa Kitanzania? Kwani tunao
wahitimu wangapi wa fani hii?" alihoji Waziri Mkuu.
"Taarifa
nilizonazo ni kwamba moja ya tishari lilidondoka baharini mkaenda
kutafuta huko na kulivuta hadi hapa ndiyo maana yameshindwa kufanya kazi
inavyotakiwa," aliongeza.
Katika majibu yake, Bw. Arika alisema wao waliagiza tishari hizo kupitia ofisi ya Bandari makao makuu ambayo iko Dar es Salaam.
"Pia wakati zinaagizwa sikuwepo hapa Tanga. Nimekuja mwishoni mwa mwaka jana," alisema Mkuu huyo wa Bandari ambaye inaelezwa alitokea Mamlaka ya Bandari Dar es Salaam.
Katika
hatua nyingine, Waziri Mkuu alimtaka Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Bibi
Mwantumu Mahiza awaite watu wa Mamlaka ya Mapato (TRA), Mamlaka ya
Bandari na Jeshi la Polisi wakae na kutafuta mbinu za kudhibiti njia za
panya zinazotumika kupitisha sukari ya magendo.
"Mkuu
wa Mkoa simamia hawa watu, msaidiane kudhibiti uingizaji wa sukari kwa
njia za panya. Kuna majahazi yanaleta sukari kutoka Brazil. Mheshimiwa
Rais amepiga marufuku uingizaji wa sukari kutoka nje ili viwanda vyetu
vya ndani viweze kuongeza uzalishaji. Dhibitini bandari zote ndogondogo
hadi Pangani," alisema Waziri Mkuu.
Alisema
changamoto inayoikabili Serikali ni kwamba hata Shirika la Viwango
Tanzania (TBS) au Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) hawawezi kuzikagua
sukari hizo na hazijulikani ubora wake licha ya kuwa zinafika kwa
walaji.
Waziri
Mkuu, Kssim Majaliwa akiongozwa na Mkuu wa Bandari ya Tanga , Henry
Arika (kulia kwake) kukagua bandari hiyo Februari 19, 2016.
Matishari
matatu ambayo Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ametaka apewe maelezo kwa
maandishi kuwa ni nani aliyeidhinisha mchakato wa manunuzi yake bila
kuzingatia viwango na ubora uliokusudiwa na serikali. mheshimiwa
Majaliwa alifanya ziara katika bandari ya Tanga Februari 19, 2016.
(Picha na ofisi ya Waziri Mkuu)
Mwenyekitiwa Baraza la Michezo Tanzania ( BMT ) Amteua Mohamed Kiganja kuwa Katibu Mtendaji Baada Ya Yule Wa Awali Kufukuzwa
Mwenyekiti
wa Baraza la Michezo Tanzania Deonis Malinzi amemteua Mohamed Kiganja
kuwa Katibu Mtendaji mpya wa baraza hilo baada ya aliyekuwa anashikilia
nafasi hiyo Bw. Henry Lihaya kutenguliwa.
Akiongea
na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam Mwenyekiti Malinzi
alieleza kuwa uteuzi huo umekuja baada ya kuona mapungufu ya utendaji
kwa aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo.
“Baraza
la Michezo Tanzania limefikia maamuzi haya baada ya kutoridhishwa na
utendaji wa Bw. Lihaya na hivyo Waziri wa habari,Utamaduni,Sanaa na
Michezo Mhe. Nape Nnauye kufanya maamuzi ya kumtengua” alisema Bw. Malinzi
Uteuzi
huo umefanyika kwa mujibu wa Sheria ya BMT namba 12 ya mwaka 1967
kifungu namba 5(1) ambacho kinampa mamlaka Mwenyekiti wa BMT kuteua
Katibu Mtendaji baada ya kupata idhini ya Waziri mwenye dhamana.
Aidha
kabla ya uteuzi huo Kiganja alikuwani Afisa Michezo Mkuu katika Ofisi
ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kuanzia mwaka
2015 mpaka uteuzi wake ulivyofanyika.
Pia
aliwahi kufanya kazi kama Afisa Mwandamizi Michezo wa Baraza la Michezo
Tanzania na Afisa Michezo Mkuu katika Ofisi wa Waziri Mkuu, anashahada
ya kwanza ya Elimu katika masuala ya Michezo na Utamaduni kutoka Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam.
Wizara Ya Mambo Ya Nje Yakanusha Kukusanya CV za Wafanyakazi Kwa Lengo la Kuwafukuza
Wizara
imepata taarifa zisizo na ukweli zinazoenezwa na kusambazwa na watu
wasiokuwa na nia njema kwa Wizara na Serikali kwa ujumla, kuwa Wizara
iliyokuwa ya Ushirikiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki iliendesha zoezi
la kukusanya wasifu(CV) za Wafanyakazi wake kwa lengo la kuwafukuza
kazi.
Wizara imesikitishwa na inalaani vikali uvumi wa taarifa hizi na inakanusha kuwa taarifa hizi hazina ukweli wowote.
Zoezi
la kukusanya CV za watumishi ni zoezi la kawaida kwa waajiri na
hufanyika Mara kwa mara kwa lengo la kuhuisha sifa na uzoefu wa
watumishi wanazopata wakiwa kazini ambapo hatimaye huwekwa kwenye
majalada yao binafsi, mwajiri anapaswa kuhakikisha jalada la kila
mtumishi lina taarifa zinazoeenda na wakati, hivyo zoezi hili
lilifanyika kwa lengo la kuhuisha taarifa za watumishi wa Wizara kama
ilivyoelekezwa na mwajiri na si vinginevyo.
Wizara
inapenda kutoa ufafanuzi kuwa CV si miongoni mwa nyaraka zinazohitajika
katika kumfukuza kazi mtumishi bali mtumishi anafukuzwa kazi kwa
kukiuka sheria, kanuni na taratibu za kiutumishi ambapo taratibu maalumu
za kinidhamu hufuatwa.
Katika
kipindi husika Wizara haina mtumishi anayetuhumiwa kwa kosa la
kinidhamu linaloweza kupelekea kufukuzwa kazi, hivyo taarifa hizi hazina
ukweli wowote.
Aidha, Wizara inakemea vikali watu wenye tabia ya kutoa taarifa zisizo na ukweli na zenye kupotosha umma.
Vilevile
Wizara inapenda kuwaasa wananchi kuheshimu sheria na taratibu za Nchi
sambamba na kutoeneza taarifa zinazotokana na vyanzo visivyokuwa rasmi
au zisizothibishwa na mamlaka husika, kwa kuwa kufanya hivyo ni kukiuka
sheria na taratibu za Nchi.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,
Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa AfrikaMashariki, Kikanda na Kimataifa.
19 Februari, 2016
Waziri Wa Fedha Na Mipango Akutana Na Wabunge Kutoka Nchini Sweden
Waziri
wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango akizungumzia vipaumbele vya
Serikali wakati wa mkutano na Wabunge kutoka nchini Sweden jana jijini
Dar es salaam kwa ziara ya kikazi nchini.
***
Waziriwa
Fedha na Mipango,Mhe. Dkt. Philip Mpango amekutana na Wabunge wa Sweden
katika ukumbi wa Wizara hiyo, kuzungumzia ushirikiano baina Tanzania na
Sweden.
Katika
mazungumzo yake na wabunge hao ambao wamewasili nchini kwa ziara ya
kikazi, Dkt. Mpango amesema Serikali ya Awamu ya Tano ipo makini na
inafanyakazi kwa ufanisi ili kuhakikisha Watanzania wanapata huduma
stahiki kutokana na rasilimali zilizopo nchini.
Amesema
Serikali imejipanga kuongeza kasi ya ukusanyaji mapato ya ndani ili
kuiwezesha nchi kujiendesha yenyewe na kuacha kutegemea misaada ya
wahisani.
Aidha,
amefafanua kuwa Tanzania imejipanga kuongeza vyanzo vya ukusanyaji
mapato pamoja na kuboresha vyanzo vilivyopo na kuhakikishakila
Mwananchi anayestahili kulipa kodi stahiki analipa kwa wakati.
“Ni
aibu kwa nchi yenye rasilimali za kutosha Wananchi wake kuishi katika
hali ya umasikini, tunachotakiwa ni kuboresha kilimo kwa sababu wananchi
wengi ndicho wanachotegemea”, alisema.
Akizungumzia
vipaumbele vya Serikali katika mkutano huo, Dkt. Mpango alisema mkazo
umewekwa zaidi katika kufanya mapinduzi ya viwanda, ambapo nchi inaanza
kuboresha viwanda vilivyopo hususani vile ambavyo hutumia rasilimali
zinazopatikana nchini kama zile zinazotokana na kilimo.
Aliongeza
kuwa katika kuboresha viwanda pia Serikali ipo katika hatua za
kuboresha soko la ndani na nje ya nchi kwa bidhaa zinazozalishwa na
viwanda hivyo.
Dkt.
Mpango alisema sambamba na kufanya mapinduzi ya viwanda, Tanzania
imejipanga kuboresha miundombinu ambapo mpaka sasa kuna miradi
mbalimbali ya maendeleo imeanzishwa kama mradi wa umeme vijijini.
Alisema
katika suala la umeme, nchi imeazimia kujikita katika uzalishaji wa
kutumia vyanzo vingine kama gesi asilia, jua na upepo kuliko kutegemea
maji pekee.
Kuhusu
sekta ya usafirishaji, Dkt. Mpango amesema Serikali imejipanga
kuboresha bandari zote nchini na kuzifanya ziwe za kisasa ili
kuhamasisha biashara za ndani na nje ya nchi kupitia bandari hizo.
Hata
hivyo, Dkt. Mpango alikiri kuwa uboreshaji wa reli ya kati ni
changamoto kwani reli hiyo haiwezi kuboreshwa kwa kutumia fedha za
bajeti ya Serikali pekee, hivyo Serikali inajitahidi kutafuta njia za
kufanikisha ujenzi huo.
Katika
mkutano huo, Dkt. Mpango alizungumzia suala la huduma za kijamii
alisema, nchi imejipanga kutoa elimu inayoendana na soko la ajira na
Serikali imeanza kutoa elimu ya msingi na sekondari bila malipo ili
kuwawezesha wananchi wengi kupata elimu.
Akizungumzia
suala la uchumi, Dkt. Mpango alisema hali ya uchumi kwa sasa ni nzuri
kwani pato la ndani la Taifa limefika asilimia 7 katika miaka ya hivi
karibuni.
Dkt.
Mpango alisema ili kufanikisha vipaumbele hivyo, ni lazima maadili na
nidhamu ya kazi vifuatwe na watendaji pamoja na watumishi wa umma katika
utekelezaji wa majukumu yao.
Aliongeza
kuwa Serikali ipo msatari wa mbele kupambana na rushwa na haitosita
kuhakikisha watu wote wanaohusika na rushwa wanachukuliwa hatua za
kisheria.
Kwa
upande Wabunge kutoka nchini Sweden, wakiongozwa na Mwenyekiti wa
Kamati ya Mambo ya Nje, Kenneth Forslund, wameipongeza Serikali ya Awamu
ya Tano kwa jitihada mbalimbali zinazochukuliwa katika ukusanyaji wa
mapato ya ndani na kutoa huduma za kijamii.
Tanzania
na Sweden zimekuwa na ushirikiano wa muda mrefu ambao umeifaidisha
Tanzania katika shughuli mbalimbali za maendeleo ikiwemo kuendeleza
miradi ya afya na umeme hususani vijijini, elimu pamoja na kusaidia
kukamilisha bajeti ya kila mwaka.
Imetollewa na Msemaji
Wizara ya Fedha na Mipango
Kitengo cha Habari
19.2.2016
Subscribe to:
Comments (Atom)
Popular Posts
-
TTCL Yakanusha Mfumo wake wa Mawasiliano Kuingiliwa.
-
Serikali Ya Tanzania Yasema Haitajitoa katika Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC)
-
TCU Yafuta Vyuo Vishiriki Vya Mtakatifu Joseph.....Wanafunzi Watakiwa Kuondoka Chuoni Mara Moja, Watapangiwa Vyuo Vingine
-
IGP Mangu Awaapisha Makamishna Wa Polisi Waliopandishwa Vyeo Na Mheshimiwa Rais
-
Rais Magufuli Asema Hataingilia Mgogoro wa Zanzibar,Ataka Wenye Malalamiko Waende Mahakamani....Hotuba Nzima Ya Rais Iko Hapa
-
Mfanyakazi Wa Kihindi Afukuzwa Kazi Nchini Kwa Kuwaita Watanzania Nyani
-
Mtuhumiwa Wa Fedha za Escrow Ajichanganya......Ni Yule Kigogo Wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA) Ambaye Alihojiwa Jana na Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma
-
Msaada Tutani: Mzazi Anatafuta Mtoto wake Aliyepotea jijini mwanza
-
Watu 5 Waliofukiwa na Kifusi Kwa Siku 41 Katika Machimbo ya Dhahabu Nyangarata Waokolewa Wakiwa Hai.
-
Uongozi wa Diamond waongea kuhusu barua ya TRA iliyosambaa mtandaoni








